Wakati aliyekuwa Mkurugenzi wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), ametajwa kutenguliwa uteuzi wake kwa kukataa kuchukua mshahara wa Serikali kwa miaka mitatu mfululizo, uchunguzi umebaini kuwa jipu la kusamehe kodi Kampuni ya Saruji ya Dangote ndilo lililomwondoa.
Uchunguzi uliofanywa umebaini kuwa mbali na Juliet Kairuki kutochukua mshahara wa Sh 5,000,000 kila mwezi aliopangiwa na Serikali kwa miaka mitatu, kwa maana kuwa ameacha kuchukua wastani wa Sh milioni 180 kwa muda huo, anatuhumiwa kusamehe Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) kwa wawakezaji bila kufuata utaratibu au sheria za nchi.
“Hili la mshahara ni cha mtoto. Amewadanganya wawekezaji wengi kuwa anaweza kuwapa msamaha wa kodi ya VAT, na sasa Serikali hii ilipoingia madarakani ikasema hana mamlaka hayo. Mwekezaji wa kwanza aliyedanganywa ni Dangote,” anasema mtoa taarifa wetu.
Uchunguzi uliofanywa umebaini kuwa Novemba, 2015 Kampuni ya Dangote iliingiza nchini makaa ya mawe tani 35,000 kutoka Afrika Kusini na kutaka makaa haya yasamehewe kodi zote.
“Kwa kweli tulishangaa sana. Kwanza, makaa ya mawe si bidhaa za mtaji (capital) bali ni za matumizi tu (consumables). Vifaa vinavyosamehewa kodi ni zile zinazotumika kuzalisha bidhaa nyingine leo, kesho, mwakani au miaka mitano ijayo na kuendelea, ila makaa ya mawe ukiyachoma yanaisha siku hiyo hiyo, hivyo hii si mtaji.
“Ukiacha hilo, hawa watu wa Dangote wameambiwa wanunue makaa ya mawe kutoka Kiwira au Ngaka, lakini hawataki,” kinasema chanzo chetu na kuongeza kuwa kwa mwaka uliopita, waliagiza tani 2,000 tu za makaa ya mawe kutoka Tancoal kinyume cha makubaliano ya kuongeza ajira nchini.
Afisa kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) amefichua katika uchunguzi huu kuwa kinachoendelea kwenye Kampuni ya Dangote ni balaa. “Hii kampuni tulidhani imekuja hapa kukomboa wananchi, lakini uhalisia siyo.
“Kampuni hii inafanya malipo bila kutoa kodi ya zuio, bidhaa inazoingiza nchini pamoja na nyingine kupata misamaha ya kodi bado inaongeza bei zinakuwa ghali mno kwa maana ya kuongeza gharama za uzalishaji na hivyo kupunguza kiasi cha kodi kinachostahili kulipwa… ni shida,” anasema afisa huyo kwa uchungu.
Kutokana na mkanganyiko huo, Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Alphayo Kidata, ameunda timu ya kufanya ukaguzi maalumu kwa Kampuni ya Dangote ambayo imewakuta na hatia.
“Hiyo bilioni 20 ni uchunguzi wa awali, tunaweza kupata kiasi kikubwa zaidi. Tunawashukuru kwa kuandika habari za ukwepaji kodi, na nakuhakikishia sisi tunafuatilia kila mnachochapisha,” anasema mtoa habari wetu.
Afisa mwingine wa TRA anasema mbinu kubwa inayotumiwa na Dangote na kampuni nyingine ambazo tayari TRA imekwishaibaini mbinu wanazotumia kupunguza faida (Tax Base Erosion), kwa kuingia mikataba yenye gharama kubwa na kampuni walizo na uhusiano nazo kibiashara, kuonesha wametumia gharama kubwa wakati uhalisia wanafanya mbinu za kukwepa kodi.
Akizungumzia sakata hili, Mejena Mkuu Mwandamizi wa Kampuni ya Dangote, Vidya Dixit, amekiri kupokea ankara ya malipo kutoka TRA yenye thamani ya bilioni 20 na akasema: “Wakaguzi wa TRA wako hapa, wamefanya uchunguzi wao, wametuletea madai yao, na sisi tunawasiliana na mshauri wetu wa masuala ya kodi, ikithibitika kuwa tunadaiwa kiasi hicho Dangote ni kampuni kubwa, tutalipa.”
Dixit amesema TRA wamekagua mikataba mbalimbali wanayotumia akina Dangote kuagiza bidhaa na huduma, na wakaja na kiasi hicho, hivyo kwake halioni kama ni tatizo, washauri wao wa masuala ya kodi wakikuta ni kweli watalipa tu. Chanzo chetu kimetueleza kuwa mshauri wao ni Kampuni ya PriceWaterhouseCoopers (PWC) ya Afrika Kusini.
Meneja huyo alijibu pia swali kuwa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TRA) inawadai dola 2,867,400 za Marekani (sawa na Sh bilioni 6.3), kwa kusema: “Mimi sisimamii idara ya uhasibu. Madeni hayo yanaweza kuwapo, ila Dangote ni kampuni kubwa, kama kuna madeni ya aina yoyote tutalipa tu baada ya kujiridhisha kuwa ni madeni halali.”
Kuhusu suala la tani 35,000 za makaa ya mawe kutoka Afrika Kusini, alisema wao kama Dangote hawapaswi kulaumiwa kwani walifuata taratibu zote: “TIC walitupa sisi msamaha wa kodi, sasa tumezungumza na Waziri wa Fedha akasema TIC hawana mamlaka ya kutoa msamaha wa kodi bila kutangaza kwenye Gazeti la Serikali (GN) na kweli hakukuwapo GN yoyote.
“Sasa hapa tunapata tabu kidogo, idara moja ya Serikali inasema hivi na idara nyingine inasema vile, tunapata shida kidogo,” anasema Dixit. Katika makaa hayo ya mawe pekee ambayo wanatakiwa kuyanunua kutoka nchini, Dangote wanadaiwa wastani wa Sh bilioni 1.1.
Kuhusu tuhuma zinazoelekezwa kwa kiwanda hicho kuwa kimewageuka wafanyabiashara wadogo na kupendelea wafanyabiashara wakubwa kwa njia ya kuwauzia saruji nyingi na kutowajali wadogo, Dixit anasema wao hawana ubaguzi na ucheleweshaji unaweza kutokea kunapotokea dharura.
Anasema kuna wakati wanaangalia nani ana ghala kubwa la kuhifadhia saruji kiasi gani, ila hiyo haiondoi ukweli kwamba hawabagui yeyote anayetaka kununua na kuuza saruji ya Dangote.
“Ukisema kuna walioshindwa kupata saruji kwa wiki moja au mbili, hilo naweza kukuelewa, lakini miezi miwili, wala asikudanganye mtu. Hilo haliwezekani. Ni kweli kule Lindi tunakotoa chokaa, machimbo yote kwa siku tatu zilizopita yalijaa maji, tukashindwa kupata chokaa, lakini zaidi ya hapo kila mtu anapewa fursa sawa ya kununua saruji bila ubaguzi,” anasema Dixit.
Awali, baadhi ya wafanyabiashara waliilalamikia Kampuni ya Dangote kuwa inauza saruji kwa upendeleo, hali inayowafanya wakose mapato kwani wamekopa mikopo benki na wanaishia kutopata saruji kwa wakati hivyo wanashindwa kulipa hiyo mikopo.
“Kuna mfanyabiashara ameweka kwenye akaunti ya Dangote Sh bilioni 2.5, huyu ndiye anayepewa saruji sisi wengine tunapuuzwa. Watanzania wengi wamekopa benki wastani wa Sh milioni 20, 30 au 50 wanaziweka kwenye kampuni ya Dangote na hawapati hiyo saruji. Hii inatutia hasara mno. Tunataka usawa katika biashara hii,” anasema mmoja wa wafanyabiashara anayedai ameweka Sh milioni 25 kwenye Kampuni ya Dangote, lakini hapatiwi saruji.
Pia, wanalalamikia bei kubwa ya saruji ya Dangote kwani wakati kiwanda kinaanza kujengwa Watanzania walitangaziwa kuwa mfuko mmoja wa saruji ungeuzwa kwa Sh 8,000, lakini sasa bei inafikia Sh 16,000 kwa mikoa kama Mwanza na kwa Dar es Salaam inauzwa kati ya Sh 10,800 na 12,500.
Kamishna Mkuu wa TRA, Kidata, hakuwa tayari kulizungumzia kwa undani suala la Dangote zaidi ya kusema: “Hili suala lipo, tunalifanyia kazi, ni mapema mno kulizungumzia kwa sasa.”
Hata hivyo, afisa mwingine mwandamizi alishangaa kusikia kuwa Dangote bado wanatafuta ushauri wa kisheria kama walipe kodi hiyo au la: “Hawa waliishakwenda hadi kwa Bwana Mkubwa wakakubali kulipa, sasa leo inakuwaje wanatafuta ushauri?” Alihoji afisa huyo.
Alichosema ni kuwa kila mfanyabiashara mkubwa kwa mdogo ajiandae kulipa kodi. “TRA haitaingilia mapato halali ya mfanyabiashara yeyote, ila kwa yeyote anayekwepa kodi hili halitavumiliki. Serikali ya sasa inasema hapa ni kazi tu, hakuna habari ya jina kubwa au dogo. Jipu ni jipu tu, bila kujali ni kubwa au dogo, yote yatakamuliwa tu.”
Ijumaa, 6 Mei 2016
Mfanyabiashara Dangote Atajwa Kutumbuliwa kwa Juliet Kairuki TIC
Wabunge wa UKAWA Wamzomea Profesa Tibaijuka huku Wakimwita Mwizi.......Ni Baada Ya Kupingana na Hoja za Tundu Lissu Aliyedai Zanzibar Ni Koloni La Tanganyika
Mbunge wa Muleba Kusini (CCM), Profesa Anna Tibaijuka jana alikuwa mkali bungeni akisema yeye si mwizi na kuwabeza wanaomuita hivyo kuwa wataisoma namba.
Profesa Tibaijuka alifikia hatua hiyo baada ya kuhamaki kutokana na baadhi ya wabunge wa upinzani kupaza sauti na kumuita mwizi wakati akichangia hotuba ya bajeti ya Wizara ya Katiba na Sheria.
Profesa Tibaijuka alianza kwa kuwataka wabunge wamuunge mkono Rais John Magufuli kwa kuwa amechaguliwa na wananchi.
“Wenzetu ambao kazi yao ni kuja kutusimamia sisi (upinzani) wana haki ya kusema wanayoyasema, lakini hata sisi tuna haki ya kuyaweka vizuri ili yaeleweke kwa wananchi,” alisema.
Profesa Tibaijuka alisema upinzani ukifilisika utabaki kukemea kwa sababu ni lazima tu useme kitu, Bunge linageuka kijiwe na bungeni si mahali pa kupeleka hoja za vijiweni.
Kauli hiyo iliwakera wabunge wa upinzani ambao walianza kupaza sauti zao dhidi yake, hali iliyoonekana kumchanganya.
Akirejea hotuba ya msemaji wa kambi ya upinzani bungeni, Tundu Lissu kuwa Tanganyika inainyonya Zanzibar na kuifanya koloni lake, Profesa Tibaijuka alihoji: “Tanganyika inainyonya Zanzibar katika lipi? Hili ni jambo la kujiuliza. Nimejiuliza mimi kama mchumi. Kazi yangu ya kwanza nyinyi mnanijua nilikuwa kwenye shirika la makazi duniani, hamjui kwamba nilikuwa kwenye Shirika la Biashara la Dunia?” alihoji.
Kutokana na zomeazomea kuendelea, Spika wa Bunge, Job Ndugai aliingilia kati: “Waheshimiwa wabunge namlinda mzungumzaji, naomba muwe wavumilivu. Mheshimiwa Profesa endelea."
“Kwa wale wanaosema nimeiba mtaisoma namba, mimi si mtu wa kutishwa na vitu vya ovyoovyo.
"Mimi sitishwi na hoja za ovyoovyo, huyo (mtu) akaisome namba. Nasimama hapa kwa sababu nataka nitetee vitu. Mtu anapopotosha anaweza kuleta hatari. Tanganyika kwa mtizamo wa kiuchumi haiwezi kuinyonya Zanzibar.
“Katika Dunia ya ustaarabu unasikia hoja. Lissu hapa angeweza kuzomewa, lakini wastaarabu wakamsikiliza wamekomaa kisiasa,” alisema huku baadhi ya wabunge wakiendelea kumzomea.
Tibaijuka aliwahi kuwa waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi wakati wa utawala wa Rais Jakaya Kikwete na aliondolewa baada ya kutuhumiwa kupata mgawo wa fedha za Tegeta Escrow.
Mwita Waitara Azusha Tafrani Bungeni.......Ni Baada ya Kutaka Kumchapa Ngumi Mbunge wa Kasulu Aliyedai Tundu Lissu na Mnyika Ni Vichaa
Mbunge wa Ukonga, Mwita Waitara (Chadema) ametolewa nje ya Bunge baada ya kutaka kumkwida Mbunge wa Kasulu Vijijini, Agustine Holle (CCM) aliyedai kuwa Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu na Mbunge wa Kibamba, John Mnyika wote wa Chadema kuwa wanaugua kichaa.
Waitara alionesha kukerwa na kauli hiyo hasa pale Holle alipokataa kufuta kauli yake, licha ya kutakiwa kufanya hivyo na Naibu Spika, Dk Tulia Akson.
Wakati Holle akichangia, Waitara alinyanyuka kwenye kiti chake na alipofika alipo mbunge huyo alimzungumzisha maneno ambayo hayakusikika na kuonesha kama kutaka kumpiga kabla ya kukaa kwenye kiti kilicho mbele yake ndipo, Holle alisikika akisema “wewe unataka nini” ndipo Naibu Spika alipogundua kuwa Waitara anataka kumpiga Holle na kumuamuru atoke nje lakini hakutii amri hiyo.
Kutokana na kutotii, Naibu Spika aliamuru askari wamtoe ndipo walipoingia zaidi ya askari watano na kutoka naye hadi nje ya geti kubwa la kuingilia bungeni.
Holle wakati anachangia bajeti ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa mwaka wa fedha 2016/2017, alimtaja Lissu ambaye ni Waziri Kivuli wa Wizara hiyo kuwa ana taarifa kuwa Lissu amewahi kuugua ugonjwa wa kichaa na hadi sasa ana faili kwenye Hospitali ya Vichaa ya Mirembe iliyopo mkoani Dodoma.
Hata hivyo, alipopewa nafasi na Naibu Spika kufuta kauli yake akasema “nafuta kauli yangu lakini kwa taarifa zilizozagaa nimeamini ni kweli na mbona kwao(Chadema) wapo wengi hata Mnyika sasa hivi yupo Muhimbili anatibiwa kichaa”.
Kutokana na kauli hiyo, Lissu alisema licha ya kuifahamu Hospitali ya Mirembe, hajawahi hata kuingia kwenye geti la hospitali hiyo wala kuugua ugonjwa huo na kutaka kiti cha Naibu Spika kimtake Holle athibitishe ; na akishindwa kanuni zielekeze hatua za kuchukua kama zilivyowekwa.
Alhamisi, 5 Mei 2016
Wabunge warushiana makonde Afrika Kusini
Wabunge nchini Afrika Kusini wamepigana bungeni baada ya spika kuamuru maafisa wa usalama kuwaondoa kwa lazima wabunge wa upinzani ambao walimbeza rais Jacob Zuma alipoingia bungeni tayari kulihutubia kikao.
Rais Zuma ambaye ameshindwa katika kesi mbili kuu zinazomhusisha na ubadhirifu wa mali ya umma na usimamizi mbaya alikuwa amefika bungeni kwa mara ya kwanza tangu kushindwa mahakamani.
Hata hivyo ujio wake uliwakera sana wabunge wa chama cha upinzani Economic Freedom Fighters (EFF).
Wabunge hao chini ya kiongozi wao Julius Malema walipiga mayowe na kumtupia matusi bw Zuma jambo lililomlazimu spika wa bunge kuamuru wabunge hao wa EFF kuondolewa nje.
Ijumaa iliyopita mahakama ya juu ya Afrika Kusini iliamua kuwa rais Zuma anapaswa kufikishwa kizimbani kufuatia kesi za ufisadi dhidi yake.
Kesi hiyo inahusiana na ufisadi uliotokea katika ununuzi wa silaha zenye thamani ya mabilioni ya dola mwaka wa 1999.
Zuma amekanusha madai yote dhidi yake, Anatarajiwa kukamilisha hatamu yake mwaka wa 2019.
Uamuzi huo wa mahakama ulikuwa msumari wa moto kwa kidonda cha Zuma ambaye mwezi uliopita alipatikana na hatia ya matumizi mabaya ya madaraka yake alipokaidi amri yakulipa pesa za umma zilizotumiwa kukarabati nyumba yake ya Nkandla.
Kampuni yatozwa Sh118 Bilioni Poda yake Kusababisha Saratani
Poda ya Johnson, iliyodhaniwa kuwa ni kipodozi na tiba mujarabu kwa watoto na watu wazima duniani kote imebainika kusababisha saratani.
Jana, Mahakama ya St Louis ya Marekani, iliiamuru kampuni inayotengeneza poda hizo, Johnson & Johnson kumlipa Deane Berg wa Sioux Falls, South Dakota, Dola za Marekani 55 milioni (Sh118 bilioni ) baada ya kujiridhisha kuwa kipodozi hicho kilimsababishia saratani ya mayai ya uzazi (ovarian cancer).
Mpaka sasa, zaidi ya wanawake 1,000 wameshafungua kesi kuishtaki kampuni hiyo kwa madai ya kuwasababishia saratani hiyo baada ya kutumia poda ya Johnson kwa miaka mingi.
Ofisa Uhusiano wa Mamlaka ya Chakula na Dawa Tanzania, (TFDA), Gaudensia Simwanza alisema wanazo taarifa juu ya madhara ya poda hizo ingawa bado hawajathibitisha kitaalamu kwa poda zilizopo nchini.
Alisema TFDA ilishafanya uchunguzi wa kimaabara kuhusu poda hizo lakini haikuona madhara yoyote.
Simwanza alisema FDA ilitakiwa pia kuwapa taarifa watumiaji wa bidhaa hizo duniani kuhusu madhara ya poda hizo.
Mwaka 2013, Berg alikuwa mwanamke wa kwanza kuishtaki kampuni hiyo baada ya kugundulika na saratani.
Baada ya kuridhishwa na malalamiko ya Berg, Mahakama iliamuru kampuni ya Johnson & Johnson kutoa onyo kuwa poda hizo, Johnson Baby Powder na sabuni ya Shower to Shower, zinasababisha saratani. Hata hivyo, kampuni hiyo haikufanya hivyo.
Baada ya mwaka mmoja, Berg alifungua tena kesi hiyo na Mahakama iliamuru alipwe kiasi hicho cha fedha.
Daktari wa Hospitali ya Wanawake, Brigham, Daniel Cramer alitoa ushahidi mbele ya Mahakama na kueleza kuwa zaidi ya wanawake 10,000 wamegundulika kuwa na saratani ya mayai ya uzazi kwenye hospitali hiyo.
Kadhalika, wanawake hao walibainika kuwa na chembechembe za ‘talcum’ kwenye kizazi.
Daktari wa Saratani wa Taasisi ya Saratani ya Ocean Road, Herry Tungaraza alisema kuna uwezekano wa kemikali ya ‘talcum’ kupenya kwenye ngozi, hadi kwenye damu na kuingia kwenye mayai ya uzazi na kisha kusababisha saratani.
Alisema si lazima poda hizi zimuathiri mtu kwa kuzitumia sehemu za siri tu, hata kama akizitumia kwa kupaka usoni, zinaweza kusafiri na kuathiri mayai ya uzazi. “Kama ingekuwa zinadhuru kwa kuzipaka sehemu za siri tu, basi zingeathiri zaidi shingo ya kizazi au nyumba ya uzazi, lakini mayai yapo mbali na ndiyo yaliyoathiriwa na saratani,” alisema.
Shahidi mwingine wa katika kesi ya Berg alithibitisha kuwa aliona chembechembe za ‘talcum kwenye uvimbe ulioko kwenye mayai ya Berg.
Mwathirika mwingine
Mei mwaka jana, Gloria Ristesund (62), alifungua kesi dhidi ya Johnson & Johnson kwa kushindwa kuwaonya wateja wake kuhusu poda hiyo kusababisha saratani.
Ristesund aligundulika na saratani, mwaka 2011 baada ya kutumia poda hiyo kwa kuipaka sehemu za siri kwa miaka kadhaa hasa. Mahakama iliamuru Ristesund pia kulipwa Dola 55 milioni.
Tovuti ya CNN inaeleza kuwa utafiti kuhusu kemikali za ‘talcum’ kusababisha saratani ulitolewa miaka mingi nyuma lakini Johnson & Johnson hawakutaka kuweka wazi ukweli huo kwa wateja wao.
“Ni kama kampuni zinazotengeneza sigara, wanajua kuwa imeshathibitishwa kuwa uvutaji wa sigara unasababisha saratani ya mapafu lakini wanauficha umma kuhusu hili,” ilisema taarifa ya CNN.
P Diddy Aongoza Orodha ya Forbes ya Wana Hip Hop Watano Wenye Mkwanja zaidi
Forbes wametoa orodha mpya ya wasanii wa hip hop wenye fedha zaidi, The Forbes Five.
Diddy ameongoza orodha hiyo mwaka huu kwa kuwa na utajiri ufikao dola milioni 750. Nafasi ya pili imekamatwa na Dr Dre mwenye dola milioni 710 huku Jay Z akifuatia kwa dola milioni 610.
Mwanzilishi wa Cash Money, Birdman amefuatia katika nafasi ya nne akiwa na dola milioni 110. Drake amechukua nafasi ya 50 Cent na kukamata nafasi ya tano kwa utajiri wa dola milioni 60.
Majibu ya Snura baada ya Chura wake Kupigwa Nyundo na Serikali
Baada ya wizara ya habari, utamaduni, sanaa na michezo kuufungia wimbo wa Snura, Chura jana, muimbaji huyo anaonesha kutoshtushwa na hatua hiyo hasa kutokana na support anaiyopata kutoka kwa mashabiki wake.
Kwa ufupi haoneshi stress, walau kwa kile alichokiandika kwenye Instagram. “Ingekua ndio hela leo ningekua bilionea lo!!! Nawapenda sana kwakweli na nawatakia usiku mwema,” aliandika Snura kwenye Instagram.
Aliongeza hashtag: #utaipenda2_ndimuimekolea_malimao_kama__210_habarizetuwanazo_ilazaohatuna.”
Pamoja na wimbo huo kufungiwa kuchezwa kwenye redio na TV, Snura aliagizwa kuhakikisha amefuta video zake zote mtandaoni.







