Jumapili, 20 Novemba 2016

Wasira: Uzee Haunizuii Kudai Haki Yangu

Waziri wa muda mrefu na mbunge wa zamani wa Bunda, Steven Wasira amewajibu wanaodai kwamba amelazimika kustaafu siasa baada ya mpinzani wake, Ester Bulaya kuwashinda wapigakura wanne waliokuwa wakipinga ushindi wake wa ubunge wa Bunda Mjini na kusema hajastaafu na uzee haumzuii mtu kudai haki yake.

Juzi, Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza ilimpa ushindi Bulaya katika kesi ya uchaguzi hali iliyotafsiriwa na wadadisi wa kisiasa kwamba huo ndiyo ulikuwa mwisho wa kisiasa wa Wasira.

Lakini jana, Wasira alipopigiwa simu na waandishi wetu kuelezea hatima yake ya kisiasa baada ya kesi hiyo, alisema wanaodai kuwa anatakiwa kustaafu siasa kwa sababu ni mzee hawana budi kuangalia kauli zao kwa sababu wapo wazee wengi anaowafahamu kwa majina na bado wapo madarakani.

“Suala la kusema nimestaafu siasa silijui na sijawahi kusema. Kesi hiyo inahusiana nini na siasa? Wapigakura wameona kuwa uchaguzi haukuwa huru na haki. Hakuna uhusiano na uhusiano uliopo ni kwa sababu mimi ni shahidi na mimi niligombea,” alisema na kuongeza:

“Nataka wanipe ‘definition’ (maana) ya kustaafu siasa. Je, ni kunyamaza, nisitoe maoni. Mbona wapo watu walikuwa wanasiasa na bado wanatoa maoni ya kisiasa tena yenye manufaa makubwa?”

Dar Mpya ya Makonda: Makonda Aitaka Takukuru Kuchunguza Madai ya Ufisadi katika Mradi wa Nyumba ‘Avic Town’

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Paul Makonda amenusa ufisadi katika mradi wa ujenzi wa nyumba za Avic ‘Avic Town’ na kuitaka taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), kuuchunguza mradi huo uliopo Kigamboni jijini humo.
makonda-new-jpg-oo

Hatua hiyo imefika baada ya kupata malalamiko kutoka kwa wananchi waliokuwa wakiishi eneo hilo na kutolewa pasipo kupewa fidia zao huku ekari 18 za Chama cha Mapinduzi (CCM),zikichukuliwa kwa matumizi katika mradi huo.

Akizungumzia hatua hiyo, Makonda amewataka watendaji wa serikali wanaohusika na taarifa za mradi huo kutoa taarifa sahihi katika vyombo vya dola kwani hataki kuona wananchi wakidhulumiwa haki zao.

“Sitaki kuona kigogo wala kijiti anahusika katika mradi huo. Nitasimamia na polisi waliohusika katika kuwatoa wananchi hawa waseme walitumia vigezo gani kuwatoa,”alisema.

Alisema wananchi walioondolewa eneo hilo wafike kwa Mkuu wao wa Wilaya huku akiitaka Takukuru kuchunguza mafaili ya mradi huo wa nyumba.

Akizungumza huku akilia mkazi wa eneo hilo ambaye pia ni mwathirika wa mradi huo, Pascalina Walioba alisema tangu mradi utambulishwe na kuanza kujengwa hawajalipwa stahiki zao.

“Mimi ni mwathirika wa mradi huo, tangu unaanzishwa na tukahamishwa kipindi hicho nilipaswa kulipwa Sh 700,000 lakini hadi leo sijalipwa na thamani ya fedha inaongezeka,”alisema na kisha kuangua kilio.

Mbunge wa Jimbo hilo, Faustine Ndungulile alisema kuwa wapo watu walikuwa wakidai kuwa ujenzi ule unahusisha nyumba za ulinzi wa usalama.

“Kuna hekari 18 za Chama cha Mapinduzi (CCM) zipo humo lakini tutalifualia,” alisisitiza Ndungulile.

Katika hatua nyingine Wilaya hiyo imeahidiwa na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), hadi kufikia February mwakani watakuwana umeme wa uhakika.

Aidha wananchi wa eneo hilo walitolewa hofu juu ya upatikanaji wa maji safi kwani tayari maji yapo ya visima lakini hakuna mabomba ya kusafirisha maji hayo.

Akizungumzia mradi wa maji katika mji huo, Mwakilishi kutoka Shirika la Maji saifi na Maji taka(Dawasco),….alisema fedha zilizotengwa katika kusambaza maji katika wilaya hiyo ni Sh bilioni 40 huku fedha zinazoitajika ili kukamilisha mradi huo ni Sh bilioni 146.