Jumapili, 5 Juni 2016

UN WAKUNWA NA KASI YA JPM


SHIRIKA la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), limeeleza kuridhishwa kwake na utendaji wa Rais John Magufuli katika mapambano ya rushwa, kuongeza uwajibikaji na ukusanyaji wa mapato.
Mwakilishi Mkazi wa UNDP nchini, Alvaro Rodriguez, alisema hayo jana katika semina ya wabunge kuhusu Malengo 17 ya Maendeleo Endelevu ya Dunia.
Alisema Serikali ya Awamu ya Tano, imekuwa ikipambana na rushwa na kusimamia kwa karibu ukusanyaji mapato, hali aliyosema itasaidia maendeleo kwa kuwa hakuna nchi iliyoendelea bila kuchapakazi.
Rodriguez alisema mbali na kuona maendeleo katika baadhi ya mikoa na mitaa, ameona jitihada hizo za Serikali na amefurahishwa na kuridhika nazo.
Mwakilishi huyo pia alisema Serikali ya Tanzania na Ofisi ya Umoja wa Mataifa (UN), zimekuwa zikifanya kazi pamoja katika harakati za usambazaji wa malengo ya dunia kwa Watanzania.
Alisisitiza umuhimu wa malengo hayo kueleweka kwa wabunge, ili katika jukumu lao la kuisimamia Serikali, wawe mabalozi wa utekelezaji wa malengo hayo katika ufuatiliaji kwenye ngazi zote za utawala.