Jumapili, 10 Mei 2015

Urais CCM waiweka pabaya kamati kuu, Mganga akutwa akiroga mahakamani na NEC yasitisha uandikishaji?

LWOOO  
MWANANCHI

Mbio za urais ndani ya CCM sasa zimefikia pabaya baada ya kuibuka hofu ya kuwapo kwa mpango wa kuivuruga Kamati Kuu kabla ya haijakutana kuchuja majina ya makada watakaotakiwa kupigiwa kura na Halmashuri Kuu ili kumpata mgombea atakayepeperusha bendera ya chama hicho kwenye Uchaguzi Mkuu.
Hadi sasa CCM haijatangaza ratiba yake kwa ajili ya kuongoza wanachama wanaotaka kuwania uongozi wa ngazi mbalimbali kwa tiketi ya chama hicho.
Hata hivyo, Kamati Kuu ya CCM itakutana Mei 20 na kufuatiwa na vikao vya siku mbili vya Halmashauri Kuu Mei 21 na 22 kwa ajili ya kupitisha ratiba, ilani na taratibu nyingine za uchaguzi, ikiwa ni kuashiria kuanza rasmi kwa mchakato wa uchaguzi ndani ya chama hicho kikongwe.
Wakati chama kikitafakari kuanzisha rasmi mchakato wa uchaguzi, tayari kuna habari kuwa moja ya makundi ya makada wanaowania urais limeonyesha kutokuwa na imani na mwenendo wa Kamati Kuu ambayo ina jukumu la kuchuja wanaowania urais na kupeleka majina Halmashauri Kuu kwa ajili ya kupigiwa kura.
Taarifa zinaeleza kuwa kundi hilo linashawishi wanachama ili wakubali kuomba kupiga kura ya kutokuwa na imani na Kamati Kuu kwa madai kuwa inaonekana kupendelea baadhi ya waliojitokeza na kubana wagombea wengine.
“Kuna mkakati wa kuweka CC itakayowasaidia kwa kuwa ukishapita hapo, umeshakuwa Rais wa nchi hii. Uzuri ukishinda ndani ya chama na kutangazwa kuwa mgombea wao, basi makundi yote hurudi kukipigania chama na wengine kujipendekeza ili wapewe nafasi katika serikali ijayo,”.
MWANANCHI
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadiki ameteua timu ya wahandisi kutoka Wilaya za Temeke, Ilala na Kinondoni kwa kushirikiana na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), kufanya tathmini ya uharibifu wa miundombinu kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha pamoja na kujua gharama stahiki kulirudisha jiji katika hali yake.
Sadiki alisema kuwa baada ya kufanya tathmini hiyo, itatoa mwanga ni kiasi gani kinahitajika ili kurudisha miundombinu iliyoharibika katika hali yake ya kawaida.
“Siwezi nikasema leo (jana) kuwa miundombinu iliyoharibikia itafanyiwa matengenezo kwa kiasi hiki au kile, subirini. Nimeitisha wahandisi na wanaendelea na kazi,” Sadiki
“ Hiki kitu siyo cha kukurupuka kina taratibu na sheria zake inabidi zifuatwe, hayo yote yakishakamilika wananchi wa mkoa huu watafahamishwa lini ukarabati unaanza na kwa kiasi gani, kwani hapa hakuna siri,”.
Alisema mvua zimelivuruga jiji na kusababisha uharibifu mkubwa wa miundombinu.
Aliyataja maeneo yaliyoathirika zaidi kutokana na mvua hizo ni pamoja na Keko, Chang’ombe Maduka Mawili, Yombo Vituka, Vingunguti, Africana, Msasani Bonde la Mpunga, Jangwani, Manzese, Kigogo, Mburahati, Boko na Basihaya.
Licha ya kuathirika na mafuriko yaliyotokana na mvua zilizoonyesha mfululizo kwa siku kadhaa, wakazi wa maeneo yaliyopatwa na adha hiyo wamesisitiza kuwa hawatahama katika makazi yao kwa sababu mafuriko yamewafuata.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti na gazeti hili walidai kuwa wameishi maeneo hayo kwa miaka mingi, wakipata huduma zote, ikiwamo maji, umeme lakini hakukuwa na adha hiyo, huku wakiitupia lawama Serikali kwa kushindwa kutafuta jinsi ya kuwasaidia.
MWANANCHI
Wakati viongozi wa vyama vya upinzani wakieleza hofu ya Uchaguzi Mkuu kuahirishwa, Tume  ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imesitisha mchakato wa kuandikisha wapigakura mkoani Mbeya uliopangwa kufanyika kuanzia Mei 5 hadi itakapotangazwa tena.
Tayari kazi hiyo inaendelea kwenye mikoa ya Lindi, Mtwara, Ruvuma na Iringa ambako kazi hiyo pia ilianza kwa kusuasua, na NEC ilitarajiwa kuongeza kasi ya uandikishaji kwa kuingia mikoa ya Dodoma, Katavi na Mbeya ambako mpango huo umesitishwa kwa muda usiojulikana.
Kaimu Mkurugenzi wa Jiji, Dk Lazaro Samweli alisema walipewa taarifa za kusitisha uandikishaji hadi hapo watapotaarifiwa tena licha ya Tume hiyo kupeleka vifaa vya BVR.
Mwezi uliopita, Nec ilitangaza kwamba ingeanza kazi hiyo ya kuboresha Daftari la Wapigakura mkoani hapa Mei 5, jambo ambalo lilisababisha uongozi wa jiji utangaze nafasi za kazi ya kuandikisha kwa wenye ujuzi wa kompyuta.
“Kabla ya Mei 4, ofisa kutoka Tume ya Uchaguzi alikuja akatuambia tusimamishe mchakato wa kuwapata watu wa kusimamia hadi hapo tutakapotaarifiwa, lakini vifaa tulishavipokea, hivyo tunawasubiri wao watakavyotuelekeza taratibu zao kwa mara nyingine tena,”Dk Samweli.
Alisema walipokea mashine 86 za BVR kutoka NEC na kwamba mashine 15 kati ya hizo ni kwa ajili ya mafunzo ya waandikishaji na 71 zinazosalia zitakuwa maalumu kwa kazi yenyewe ya kuandikishia.
Viongozi wa vyama vya upinzani wamekuwa wakituhumu kuwa kusuasua huko kwa kazi ya kuboresha Daftari la Wapigakura ni mpango wa kutaka Serikali ya Awamu ya Nne iongezewa muda kwa kuwa haijajiandaa kukabidhi madaraka.
Mwenyekiti wa NEC, Jaji Damian Lubuva alisema hakuwa na taarifa za kusitishwa kwa uandikishaji mkoani Mbeya, lakini akaongeza kuwa wananchi wanatakiwa kuwa wavumilivu kwani uandikishaji utafanyika kama ulilovyopangwa.
Unajua sikuwa na taarifa hizo kwa sababu nilikuwa katika kikao na wenyeviti wenzangu wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC). Kama kweli limesitishwa, itakuwa ni mchakato mdogo wa maandalizi haujakamilika. Ila niwatoe hofu wakazi wa mkoa huo uandikishaji utafanyika kama ulivyopangwa,” Jaji Lubuva.
MWANANCHI
Siku moja baada ya Ikulu kutangaza kuwasafisha mawaziri watano na Katibu Mkuu, Eliackim Maswi, wabunge wamejiweka pembeni na suala hilo wakisema Bunge lilishatimiza wajibu wake.
Juzi, Ikulu iliwasafisha mawaziri wanne walioshinikizwa kuachia ngazi na Bunge kutokana na kuhusishwa na sakata la Operesheni Tokomeza Ujangili na mmoja aliyejiuzulu kutokana na kashfa ya uchotwaji wa Sh306 bilioni kutoka Akaunti ya Tegeta Escrow, pamoja na katibu mkuu wa wizara.
Waliotangazwa na Ikulu kuwa safi ni Emmanuel Nchimbi, aliyekuwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa na Shamsi Vuai Nahodha, aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani. Wawili hao wanatajwa kwenye kinyang’anyiro cha urais kwa tiketi ya CCM ingawa hawajatangaza nia.
Wengine ni aliyekuwa Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Hamis Kagasheki na aliyekuwa Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, David Mathayo.
Hali kadhalika, Profesa Sopster Muhongo aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini ambaye alijiuzulu kutokana na kashfa ya escrow, pamoja na katibu mkuu wa wizara hiyo, Eliackim Maswi aliyesimamishwa kutokana na sakata hilo, wametangazwa kuwa safi.
Waziri Kivuli wa Maliasili na Utalii, Mchungaji Peter Msigwa alisema kitendo cha Serikali kutangaza kuwa mawaziri hao hawakuhusika katika kutekeleza makosa yaliyotokana na Operesheni Tokomeza, kinaonyesha nia ya kuendeleza tabia ya viongozi kutopenda matatizo yaliyotokea wakiwa madarakani.
“Kilichofanyika ni kuionyesha dunia kuwa hakuna kuwajibika, unapopewa jukumu lazima uwajibike. Sijui Taifa hili linakwenda wapi? Nakosa hata maneno ya kuzungumza,” Msigwa.
Mbunge wa viti maalumu (CCM), Esther Bulaya alisema kuwa katika taarifa hakuna kipya kwani haina tofauti na ile ya Kamati ya Bunge iliyoundwa kuchunguza suala hilo.
“Jana (juzi) nilimsikiliza kwa makini sana (Katibu Mkuu Kiongozi) Balozi Sefue wakati akitoa taarifa hiyo kwa waandishi wa habari ila kichwani lilinijia swali moja tu; hivi madai yaliyotolewa na wananchi katika tume iliyoundwa kuchunguza jambo hili ya kweli au si kweli?” Bulaya.