MAPYAA!
 Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrati (DP), Abdul Juma Mluya 
ameibuka na kusema mazingira ya kifo cha aliyekuwa mwenyekiti wa chama 
hicho, Mchungaji Christopher Mtikila yamejaa utata huku akiweka wazi 
kwamba, inavyoonekana aliuawa kabla ya ajali yenyewe.
Mtikila 
alifariki dunia katika ajali ya gari aina ya Toyota Corolla namba T189 
ARG, Oktoba 4, 2015 iliyotokea kwenye Kijiji cha Msolwa, Bagamoyo, 
Pwani. Wengine watatu walijeruhiwa.
Mti ambao gari liliugonga kwa juu kabla ya kupinduka.
Akizungumza na Uwazi mwishoni
 mwa wiki iliyopita kwenye ofisi ndogo ya chama hicho nyumbani kwa 
marehemu, Mikocheni B jijini Dar, Mluya alisema hata watu waongee vipi, 
lakini uchunguzi wao umeonesha kwamba, kiongozi wao aliuawa tofauti na 
eneo la ajali na mwili kwenda kutupwa pale.
ROHO YAKE ILIWINDWA KWA SIKU 40
Mluya alisema:
 “Ndugu mwandishi, Mchungaji Mtikila kama kufa alikuwa afe muda mrefu 
sana pengine siku arobaini zilizopita (mpaka siku ya kifo cha kweli), 
kwa sababu amewindwa na watu ambao hatujajua lengo lao kubwa lilikuwa 
nini!
“Kila alikokwenda kwa shughuli za kichama kulikuwa na timu ya watu inayomfuatilia.”
...Baada ya Kupinduka
MARA YA KWANZA
“Tarehe 
siikumbuki, lakini ni Septemba mwanzoni. Tulikuwa Bunda, Mara kwenye 
shughuli za chama, kuna watu ambao walikuwa hawaeleweki walitufuata 
mpaka hotelini.
“Baada ya kubaini hilo, nilimuuliza mwenyekiti kuhusu ratiba aliyokuwa nayo ya kuzungumza kwenye runinga ya Staa TV.
“Alinipa 
ratiba. Baada ya kumaliza kuzungumza, nilimwambia Bunda si mahali pa 
kulala hivyo nilimshauri aondoke, aende Mwanza. Na nilimwambia dereva 
wake aondoke bila kuaga.”
WAKIWA NJIANI
“Lakini cha 
ajabu, wakiwa njiani wakielekea Mwanza kuna gari liliwafuata kwa nyuma 
kwa mwendo ambao waliutulia shaka. Dereva wa mwenyekiti alipokuwa 
akiongeza mwendo, naye anaongeza, akipunguza naye anapunguza.
“Ilibidi dereva amwambie mwenyekiti naye akamtaka dereva aongeze kasi hadi Mwanza.”
“Katika ratiba
 yetu tulitaka kufanya ziara za kichama kuanzia  Oktoba 18,  mwaka huu 
kwa kuanzia mkoa wa Kigoma na kwingineko. Pamoja na kufuatiliwa kote 
kule mwenyekiti hakuwa na roho ya uoga hata kidogo. Alimtanguliza sana 
Mungu.
“Kwa hiyo wasiwasi mkubwa wa kufuatiliwa na watu hao ulianza Mara na Mwanza kwa nyakati tofauti.
“Septemba 11, 
mwaka huu ndiyo tarehe ambayo sasa nilianza kukariri matukio hayo hatua 
kwa hatua. Siku hiyo tulikwenda kwenye Kijiji cha Usangu mkoani Pwani 
kwa ajili ya kufanya kampeni ya mgombea udiwani. Baada ya kumaliza 
tuliamua kurudi Dar lakini njiani dereva akasema kuna watu hawajui 
wanakuja nyuma yetu.”
WAPOTEA NJIA KWA KUFUATILIWA
“Tulijikuta 
tukipotea njia na kutokea mjini Kisarawe (Pwani). Pale tulifika kituo 
cha mafuta ambapo tulikuta gari aina Toyota Land Cruiser VX limepaki 
kama vile ni watu pia walikuwa wakitufuatilia.
“Lengo la 
kusimama pale lilikuwa kupata chakula lakini hatukufanya hivyo kulingana
 na mazingira. Tukaanza safari ya kurudi Dar. Tulipofika Pugu Sekondari,
 gari lile lilitupita kwa kasi na kupotea.
“Tulipofika 
Tazara gari lile lilionekana na wakati huo yalikuwa mawili. 
Kilichotushangaza ni upya wa magari lakini eti namba zinaanzia na A. 
Mimi nilifikiria kwamba, pengine ni za idara  ya  usalama  wa  taifa  
zilikuwa doria  mbalimbali hasa kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi.
“Ndugu mwandishi, mimi ninafanya kazi ya siasa, niko makini sana. Niliwaambia wenzangu kuwa tunafuatiliwa.
“Ndani ya gari
 sisi tulikuwa na viongozi wa kuwapeleka Temeke. Lakini baada ya kufika 
huko lile VX tulikutana nalo. Tulipomuacha yule tuliyempeleka kule, 
tukawa tunampeleka mchungaji nyumbani kwake (Mikocheni) lakini bado lile
 gari lilikuwa likitufuatilia.”
WAPIGA CHENGA
“Tulipofika 
maeneo ya Msasani kwa Mwalimu (Julius Nyerere) dereva alikunja kona 
kuelekea kwa mchungaji na lile gari likakunja kona na kurudi 
lilikotoka.”
SIKU NYINGINE
“Siku 
iliyofuata tulipanga mipango yote ambapo sasa tulisema Oktoba 18, mwezi 
huu tuanze ziara ya mkoa wa Kigoma  na maeneo  mengine ya Kanda ya Ziwa.
“Mimi 
niliondoka kuelekea Shinyanga, yeye (Mchungaji) aliandaa safari ya 
kwenda Njombe kwenye kampeni ya mgombea Ubunge Jimbo la Njombe.”
OKTOBA 2, 3, 2015
“Mwenyekiti 
aliondoka Dar Oktoba 2, kuelekea Njombe. Oktoba 3, alinipigia simu 
asubuhi na kunijulisha kuwa  jana yake walipata ajali maeneo ya 
Makambako wakati wanakwenda.
“Nilimuuliza alipata matibabu, akajibu kuna viongozi wa Njombe walifika na kumchukua hivyo yuko sawasawa.”
TAARIFA YA AJALI
“Siku hiyo 
hiyo walifanya kampeni na jioni yake walianza safari ya kurejea Dar. 
Walipofika Mkoa wa Pwani, saa kumi na moja alfajiri, Mchungaji Mgaya 
alinipigia simu na kuniambia walikuwa njiani wanarudi Dar, wamepata 
ajali mbaya sana. Lakini hakuniambia kama mchungaji amefariki dunia.
“Nilianza 
kufuatilia tukio hilo na kuuliza kama kuna msaada wowote wameupata, 
akasema mpaka muda huo polisi walikuwa hawajafika. Mimi napenda sana 
kufungua mitandao ya kijamii, nilipofungua nikakuta picha zilishasambaa 
kwenye mitandao kitu ambacho nilijiuliza usiku huo huyo mpigapicha 
alikuwa wapi?”
SHAKA KUBWA YA DP
“Sisi DP, 
mashaka yetu makubwa ni mazingira mazima ya namna kiongozi huyo 
alivyofariki dunia. Hata mtoto hawezi kudanganywa kwa namna hiyo. DP ina
 taasisi ya kufanya uchunguzi iitwayo Liberty International Foundation 
iliyokuwa ikisimamiwa na marehemu. Ipo kazini kwa sasa ili kubaini 
ukweli wa kifo cha mwenyekiti na tutaweka wazi kila kitu.”
“Laini pia tunaitaka serikali kufanya uchunguzi na kutoa taarifa hadharani.”
MWENYEKITI KIJIJI AIBUKA NA YAKE
Uwazi pia lilifika aneo la ajali na kujionea kwa macho mazingira yake na kupata maelezo kutoka kwa baadhi ya mashuhuda.
Joshua Mohamed
 Msigala ni Mwenyekiti wa Kijiji cha Msolwa, Chalinze, Pwani palipotokea
 ajali. Yeye anasimulia mambo aliyoelezwa na mmoja wa majeruhi, 
Mchungaji Patrick Mgaya siku ya tukio.
“Kwanza kabisa
 waandishi wa habari mmefanya vizuri kufika eneo la tukio na kujionea 
hali halisi. Nawaeleza hali halisi ilivyokuwa mpaka mimi kufika eneo la 
ajali.
“Siku hiyo 
asubuhi ya saa kumi na moja na nusu kama sikosei, nikiwa nyumbani 
nilipigiwa simu na dereva mmoja wa lori anayenijua. Akasema ameona ajali
 maeneo yangu lakini hajui kama kuna waliokufa au la!”
MWENYEKITI AWAHI NA BODABODA
“Kusikia 
hivyo, nilichukua bodaboda ili niwahi. Nilifika ndani ya dakika kama 
kumi tangu kutokea kwa ajali. Nilikuta mwili wa Mtikila umelala pembeni 
ya gari huku wengine watatu waliodai walikuwa ndani ya gari wakiwa 
wamesimama tu.
“Ila kati ya hao watatu, mmoja alijitambulisha kuwa ni Mchungaji Mgaya, yeye wakati nafika alikuwa akiongea kwa simu.”
ALICHOAMBIWA NA MCHUNGAJI
“Nilimuuliza 
mchungaji ilikuwaje? Akasema wakati wanapata ajali hiyo, marehemu 
Mtikila na wengine wawili walichomoka ndani ya gari hali iliyosababisha 
kifo cha Mtikila. Hata hivyo, kwa upande wangu sikuamini kama wote 
walichomoka kutoka kwenye gari bali mazingira yalionesha walitoka 
wenyewe.
“Mchungaji 
alizidi kuniambia kuwa, gari lilipaa juu zaidi ya futi kumi na kugonga 
mti kisha likapinduka na kulalia paa (kwenye Uwazi siku ya tukio, 
mchungaji alisema gari lilibiringika).
“Lakini pia 
siamini, kwani pamoja na kuona alama katika mti sikubali kama 
zilisababishwa na ajali kwani kama ni hivyo gari lingekuwa limepondeka 
zaidi juu lilikoangukia tofauti na lilivyokuwa likionekana.”
KILICHOMSHANGAZA ZAIDI MWENYEKITI
Mwenyekiti 
huyo alizidi kusimulia kushangaa kwake: “Kitu kingine kinachonishangaza 
ni kwamba, kwa maelezo yao gari liliacha barabara likawa linaendeshwa 
pembeni kwa umbali wa meta mia moja (urefu wa uwanja wa mpira). Kwa nini
 dereva asipunguze mwendo ambapo angefanya hivyo gari lisingefika kwenye
 mti.”
“Kinachoshangaza
 kingine ni kwamba, hakuna majeraha yaliyoonekana kwa macho kwa 
walionusurika hata kuonesha kwamba walikatwa na vioo wakati wakirushwa 
nje kutoka ndani ya gari. Hata viti vya mbele vilikuwa vilevile, 
havikuharibika na kama majeruhi walirushwa nje walipitia wapi?”
WALIOFIKA AWALI
Mwenyekiti 
huyo alisema anawashukuru askari wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi Tanzania
 (JWTZ) wa Kambi ya Kizuka na Sangasanga waliokuwa wakipita ambapo 
walifika kutoa msaada.
“Baadaye mimi 
nilifanya mawasiliano na Polisi wa Kituo cha Chalinze (Bagamoyo) ambapo 
walifika eneo la tukio. Pia polisi wa mkoa nao walifika na saa 12:30 
asubuhi majeruhi na mwili wa marehemu walipelekwa Hospitali Teule ya 
Rufaa Tumbi.”
Naye Ofisa 
Mtendaji wa Kijiji cha Msolwa, Joseph Hamad kwa upande wake alisema 
alipokea taarifa saa 3 asubuhi na alipowasiliana na mwenyekiti 
alimwambia yupo katika eneo la tukio.
Baadhi ya 
wananchi wa kijiji hicho waliohojiwa na Uwazi walisema wameshangazwa na 
ajali hiyo iliyosababisha kifo cha Mchungaji Mtikila na kuitaka serikali
 kufanya uchunguzi wa kina.
SIMU YA MTIKILA YAZUA UTATA
Mpaka 
tunakwenda mitamboni, familia ya Mtikila ilisema, jana ilitarajia 
kufuatilia simu ya marehemu kwani haijulikani ilipo na pia kujua walipo 
dereva (George Ponella) na msaidizi wake (Ally Mohamed) ambapo awali, 
dereva alishikiliwa na jeshi la polisi.
Habari imekusanywa na Makongoro Going, Haruni Sanchawa na Issa Mnali.
Source:GPL







0 comments:
Chapisha Maoni