 WAKATI wapinzani wakipinga uteuzi wa Waziri wa Nishati na 
Madini, Profesa Sospeter Muhongo, waziri huyo amewasihi wananchi 
kumvumilia kidogo, ili baada ya muda mfupi atoe mpango wa maendeleo ya 
wizara hiyo, ambao pamoja na mambo mengine, utaelezea bei ya nishati 
hiyo itakavyoshuka.
WAKATI wapinzani wakipinga uteuzi wa Waziri wa Nishati na 
Madini, Profesa Sospeter Muhongo, waziri huyo amewasihi wananchi 
kumvumilia kidogo, ili baada ya muda mfupi atoe mpango wa maendeleo ya 
wizara hiyo, ambao pamoja na mambo mengine, utaelezea bei ya nishati 
hiyo itakavyoshuka. 
Akizungumza na waandishi wa habari muda mfupi baada ya 
kuapishwa kushika wadhifa huo jana Ikulu jijini Dar es Salaam, Profesa 
Muhongo alisema mbali na mkakati wa kushusha bei ya umeme, kasi ya 
kusambaza umeme vijijini kupitia miradi ya Wakala wa Nishati Vijijini 
(REA), itarejea palepale.
“Nimepokea uteuzi huo, kinachofuata ni kuwatumikia 
wananchi, niwaombe tu wanivumilie kidogo nitawapa mpango wangu wa 
maendeleo wa muda mfupi na mrefu, lakini nisisitize tu nishati sio 
siasa, ni suala la utaalamu, liachwe lifanywe kitaalamu,” alisema Profesa Muhongo.
Akizungumzia bei ya umeme na upatikanaji wake, Profesa 
Muhongo alisema kupunguza bei hiyo ni ajenda muhimu itakayozingatiwa na 
kusema ili umeme uwe wa uhakika, ni lazima kuwe na mipango ya kuwa na 
nishati hiyo ya uhakika ifikapo mwaka 2025.
“Umeme wa uhakika utapatikana na matarajio yetu ni 
Tanzania kuwa nchi ya uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025 ambapo 
tunatarajia uzalishaji wa nishati hiyo ufike Megawati 10,000 hadi 
15,000,”alisema Profesa Muhongo.
Alisisitiza kwamba wizara yake haitategemea chanzo kimoja 
cha nishati bali wataangalia vyanzo vingine ikiwemo nishati jadidifu, 
upepo, gesi, makaa ya mawe, maji huku akisema vyanzo hivyo vikitumika 
kuzalisha nishati, ni wazi bei ya umeme itashuka na kushusha gharama 
nyingine za maisha na za uwekezaji.
Aliongeza katika kuendeleza sekta ya nishati suala la 
uwekezaji ni muhimu hivyo wizara yake inakaribisha wawekezaji wenye 
sifa, watakaowekeza kwenye sekta hiyo ili kuja na matokeo bora zaidi, 
wananchi wanufaike na rasilimali za nchi yao.
Pamoja na nia yake hiyo kwa wananchi, Profesa Muhongo 
anakabiliwa na pingamizi kutoka kwa wanasiasa wa vyama vya upinzani, 
akiwemo Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu (Chadema) na aliyekuwa 
Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba.
Lissu na Profesa Lipumba, wamekaririwa wakikosoa uteuzi wa 
Profesa Muhongo kwa madai kuwa wizara aliyopewa kuiongoza, ilikumbwa na 
kashfa ya Akaunti ya Tegeta Escrow wakati wa uongozi wake, ikasababisha 
ajiuzulu.
Hata hivyo, Profesa Lipumba na Lissu katika kukosoa huko, 
hawakutaka kutumia kumbukumbu zilizo wazi kuwa uchunguzi dhidi ya 
Profesa Muhongo, ulibaini kuwa hakukiuka maadili yoyote katika sakata la
 utoaji wa karibu Sh bilioni 300 zilizokuwa katika akaunti ya Tegeta 
Escrow, iliyokuwa Benki Kuu (BoT).
Matokeo ya uchunguzi huo yalitangazwa Mei mwaka huu na 
Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue, ambapo alisema Tume ya 
Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma, ndiyo ilifanya uchunguzi 
kama Profesa Muhongo alistahili kwenda kwenye Baraza la Maadili kujibu 
mashitaka, lakini hawakuona tatizo lake na kufunga shauri lake.
Balozi Sefue aliweka wazi kuwa Profesa Muhongo alijiuzulu 
kwa sababu za kisiasa, lakini kimaadili hakuhusika kwa namna yoyote, 
kutokana na uchunguzi wa Sekretarieti ndiyo sababu hakufikishwa katika 
Baraza la Maadili.
Kitu kingine ambacho Lissu na Profesa Lipumba, hawakutaka 
kuzungumzia ni utendaji wa Profesa Muhongo alipokuwa katika wizara 
wakati wa uongozi wa Serikali ya Awamu ya Nne, chini ya Rais mstaafu 
Jakaya Kikwete.
Kumbukumbu zinaonesha kuwa katika miaka miwili ya uongozi 
wake katika Wizara ya Nishati na Madini, Profesa Muhongo alisimamia kwa 
umahiri usambazaji wa umeme vijijini. 
Kabla ya kuteuliwa kwa Profesa Muhongo, Watanzania asilimia
 14 tu ndio waliokuwa wakitumia nishati ya umeme, kati yao asilimia 12 
walikuwa watumiaji wa mijini na asilimia mbili ndio walikuwa watumiaji 
wa vijijini.
Kwa mujibu wa takwimu za Serikali, kati ya mwaka 2007 na 
mwaka 2010, kulikuwa na ongezeko la asilimia nne la watumiaji wa umeme, 
hali iliyoonesha kuwa ongezeko la Watanzania waliokuwa wakipata umeme, 
lilikuwa asilimia moja kwa mwaka. 
Lakini baada ya kuteuliwa kwa Profesa Muhongo katika nafasi
 hiyo, katika muda mfupi wa uongozi wake, idadi ya Watanzania wanaotumia
 umeme iliongezeka na kufikia asilimia 36 katikati ya mwaka jana.
Kwa hatua hiyo, uongozi wa Profesa Muhongo ulivuka malengo 
ya Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambayo ndio msingi wa utekelezaji
 wa malengo ya Serikali, iliyotaka Serikali kuhakikisha ifikapo mwaka 
2015, asilimia 30 ya Watanzania wawe wanapata umeme.
 Katika kutimiza malengo ya Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 
2010, uongozi wa Profesa Muhongo, ulitangaza punguzo la gharama za 
kuunganisha umeme majumbani kutoka Sh 177,000 za awali hadi Sh 27,000 
vijijini.
Awali, punguzo hilo lilitolewa kwa mikoa ya Lindi na 
Mtwara, ambako bomba la kusafirisha gesi kwenda Dar es Salaam limeanzia 
na limepita, lakini baada ya muda gharama hizo zilishushwa kwa vijiji 
vyote nchi nzima.
Profesa Muhongo mwenyewe alikaririwa akisema gharama hizo 
zitahusu miradi inayosimamiwa na Wakala wa Umeme Vijijini (REA), katika 
kipindi ambacho makandarasi watakuwa wakiendelea na awamu ya pili ya 
miradi iliyoanza Machi mwaka huu na kutarajiwa kukamilika katikati ya 
mwakani.






 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
0 comments:
Chapisha Maoni