CHAMA CHA DEMOKRASIA NA MAENDELEO (CHADEMA)
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI JUU YA MAAZIMIO YA KIKAO CHA KAMATI NDOGO YA KAMATI KUU
1.0 UTANGULIZI
Kikao cha Kamati Ndogo ya Kamati Kuu cha dharura kilichoketi tarehe 14 
Februari, 2017 Jijini Dar es Salaam katika Hoteli ya Bahari Beach 
kilipata nafasi ya kujadiliana kwa kina kuhusu matukio mbalimbali 
yanayoeendelea hapa nchini ikiwa ni pamoja na kutolewa kwa kauli 
mbalimbali na viongozi wa kiserikali na ambazo zimeendelea 
kuuthibitishia umma wa watanzania kuwa nchi yetu haiendeshwi kwa misingi
 ya kuzingatia Katiba, Sheria na Kanuni tulizojiwekea kama Taifa .
Aidha Kamati hiyo ilipata muda wa kutafakari kwa kina zaidi juu ya 
Operesheni UKUTA ambayo tumeendelea kufanikiwa katika kuitekeleza kwa 
vitendo na pia watanzania wengi zaidi sasa wameona umuhimu wa kuendelea 
na Operesheni UKUTA kwani Taifa linaelekea kwenye kutumbukia kwenye 
utawala wa kutokufuata Katiba na Sheria za Nchi (Udikteta kamili).
Mwalimu Nyerere Julai 19, 1967 alisema hivi kuhusu udikteta “Udikteta
 ni serikali ya mtu mmoja au kikundi cha watu wachache na wao ndiyo huwa
 sheria.Anayepinga watakayo,basi huonyeshwa cha mtema kuni”
Kamati hiyo imejiridhisha bila shaka kuwa sasa Chama chetu kinawindwa na
 watawala pamoja na Rais Mwenyewe na hii ni katika kuelekea kufikia 
lengo la Rais alilolitangaza alipokuwa Singida mwezi Juni ,2016 ya 
kuhakikisha kuwa upinzani unakufa ,ifikapo au kabla ya mwaka 2020.
Aidha Kamati hiyo imejiridhisha bila shaka ya kuwa sasa zinatengenezwa 
chuki za makusudi baina ya vyombo vya dola na wananchi . Hii inatokana 
na ukweli kuwa Amiri Jeshi Mkuu alisikika akiagiza Polisi wawe na 
utaratibu unaofanana na Jeshi la Wananchi. Hii ina maana kwamba Polisi 
lisiwe tena ni jeshi la kulinda wananchi na mali zao bali ni jeshi la 
kuilinda serikali .
Tumeshaona tayari Polisi wamepiga marufuku (Tamko la Advera –msemaji wa 
jeshi la Polisi) wananchi kwenda kuwatembelea ndugu , jamaa na marafiki 
wanapokuwa katika vituo vya polisi bila hata kutaja kifungu cha sheria 
kinachowapa mamlaka hayo.
2.0 KAMATAKAMATA NA FUNGAFUNGA YA WAPINZANI
Mara baada ya Uchaguzi Mkuu wa 2015 viongozi na wanachama wa CHADEMA 
wamekuwa wakikamatwa na kushtakiwa kwa makosa ya kubambikiziwa kwa 
kisingizio cha uchochezi na mpaka sasa kuna jumla ya wanachama na 
viongozi 215 ambao wamefunguliwa kesi zaidi ya 78 katika nchi nzima 
.Wengi wao wamenyimwa dhamana bila sababu za msingi . Na wale ambao 
walipatikana na hatia walipewa adhabu za vifungo bila ya kupewa fursa ya
 faini.
Hivi sasa umekuwa ni mtindo kwa mahakama kuwakatalia dhamana wanachama 
wa CHADEMA bila ya sababu za msingi.Pia imekuwa ni mtindo kuwahukumu 
vifungo bila kuwapa fursa ya kulipa faini.
Tumeamua na tunandaa orodha kamili itakayoainisha kesi zote za jinai 
ambazo ziko mahakamani na kuonyesha aina ya mashtaka na vifungo 
vilivyotolewa ambayo itawekwa wazi kwa vyombo vya habari na taasisi za 
ndani na nje ya nchi kuthibitisha kuwa kuna mpango wa kuwafunga viongozi
 wa upinzani kwa kusudi ili kuudhoofisha upinzani.
3.0 VITUKO VYA MKUU WA MKOA WA DAR ES SALAAM KUTANGAZA MAJINA YA WATU HADHARANI KUWA WANAHUSIKA NA DAWA ZA KULEVYA
Chama kinaunga mkono jitihada za dhati za kupambana na madawa ya kulevya
 nchini, kama sheria na taratibu tulizojiwekea zitafuatwa kikamilifu 
wakati wa mapambano hayo.
Kamati kuu inalaani kwa nguvu zote kitendo cha Mkuu wa Mkoa wa Dar es 
Salaam (Paul Makonda) kutangaza majina ya watu mbele ya vyombo vya 
habari na kuwatuhumu kuwa ama wanahusika katika kusambaza, kuuza au 
kutumia madawa ya kulevya kwa lengo la kuwachafulia majina, 
kuwadhalilisha,kuwafedhehesha na kuwaondolea heshima yao kwa umma 
.Tunalaani kitendo hiki kwa sababu zifuatazo:
i. Mkuu wa Mkoa amekiuka masharti ya Katiba ibara ya 13(6) (b) na (e) 
ambavyo vinaweka bayana kuwa mtu hatachukuliwa kuwa ametenda kosa la 
jinai mpaka itakapothibitika kuwa anayo hatia ya kosa hilo na kuwa ni 
marufuku kwa mtu kuteswa ,kuathibiwa kinyama au kupewa adhabu 
zinazomtweza au kumdhalilisha
ii. Mkuu wa Mkoa amekiuka kifungu cha 54 cha Sheria ya Mwenendo wa Mashtaka ya Jinai
iii. Mkuu wa Mkoa hana mamlaka kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge
 inayompa kazi na majukumu yake yaani ‘sheria ya Tawala za Mikoa ya 
1997’ kuwa ana wajibu wa kutaja majina ya watu anaowatuhumu kuhusika na 
madawa ya kulevya .
iv. Mkuu wa Mkoa alikiuka ‘sheria ya Kuthibiti na kupambana na dawa za 
Kulevya,2015’ ambayo haimpi mamlaka ya kutangaza na au kuwataka watu 
ambao yeye anawatuhumu kujihusisha na usambazaji, uuzaji na au utumiaji 
wa dawa za kulevya kufika katika vituo vya Polisi .
v. Mkuu wa Mkoa alienda kinyume kabisa na mila na desturi za Kitanzania 
,kuwachafulia watu majina na kuwadhalilisha mbele ya jamii huku akijua 
kuwa hawezi kuwasafisha na wengine ni viongozi wa dini ambao wanaaminiwa
 na waumini wao .
4.0 HATUA 
a. Kamati hiyo inaunga mkono hatua ya Mwenyekiti wetu Taifa 
Mhe.Freeman Mbowe (MB) ya kumfungulia kesi ya Kikatiba na ya Madai Paulo
 Makonda katika Mahakama Kuu ya Tanzania na itaungana naye katika kesi 
hiyo kwa kumpatia mawakili wa Chama .
b. Aidha inatoa wito kwa wale wengine wote ambao walitajwa na wanaamini 
kuwa walionewa,kuchafuliwa majina na au kudhalilishwa wafungue mashauri 
mahakamani , kwani hii ndio njia pekee ya kuzuia wengine wasifanyiwe 
uonevu kama huu siku zijazo.
c. Kamati hiyo inawapongeza kwa dhati kabisa wabunge wote wa Bunge la 
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kukubaliana, kuungana na kuweka 
itikadi za vyama vyao pembeni wakati wa mjadala wa kulinda hadhi na 
madaraka ya Bunge. Inatoa rai kuwa waendeleze moyo huohuo kwa siku 
zijazo kwa maslahi mapana ya Taifa letu.
5.0 HITIMISHO.
Kamati hiyo inatoa wito ufuatao kwa viongozi, asasi za Serikali, 
wananchi wazalendo na wanachama wa CHADEMA, kufanya mambo yafuatayo;
1. Viongozi wana wajibu wa kuitetea , 
kuilinda na kuitekeleza Katiba ya Jamhuri ya Muungano na Sheria za Nchi.
 Mwalimu Nyerere aliwahi kutuasa kuwa Rais asiyeweza kuilinda,kuitetea 
na kuihifadhi Katiba hatufai.
2. Mahakama Itekeleze wajibu wake kwa 
weledi uliotukuka kuhakikisha kuwa haki sio tu inatendeka bali 
inaonekana kutendeka bila ya vitisho kwake kutoka kwa mtu yeyote.Iige 
mfano wa uhuru wa mahakama na weledi wa Majaji wa Afrika ya Kusini, 
Zimbabwe na Marekani ambao waliweza kutengua amri batili zilizotolewa na
 Marais wa nchi zao.
3. Polisi na Jeshi la Wananchi wa Tanzania watekeleze
 majukumu yao kwa weledi kwa mujibu wa sheria na taratibu 
zilizowekwa.Wasikubali kuwaonea watu kwa misingi ya Vyama ,Itikadi au 
misimamo yao.Polisi Wajibu wao Kisheria ni kulinda usalama wa raia na 
mali zao , Jeshi la Wananchi wa Tanzania wajibu wao Kikatiba ni kulinda 
mipaka ya Nchi.
4. Mawakili wana wajibu mkubwa kuisaidia
 mahakama kutekeleza majukumu yake kwa weledi kuhakikisha haki 
inatendeka bila woga ,vitisho au vishawishi .Wasikubali kutishwa na mtu 
au asasi yeyote katika kuitetea ,kuilinda na kuitekeleza Katiba na 
Sheria za Nchi.
5. Wasomi na wanataaluma wana wajibu wa 
kutambua na kuitikia mwito wao wa kutetea ukweli na kulinda haki za 
jamii hata kama kwa kufanya hivyo kutaathiri maslahi yao binafsi
6. Wanachama tuendelee kudai demokrasia 
kwa nguvu zote bila woga kwa mujibu wa Katiba na sheria za 
Nchi.Tushikamane kukikuza Chama kuanzia ngazi ya Misingi hadi Taifa 
kuendelea na Operesheni UKUTA .
7. Wananchi nchi hii ni yetu sote ni 
lazima tufaidike nayo kwa mujibu wa Katiba na Sheria za nchi bila 
vitisho .Tuungane kudai demokrasia na uhuru wa kweli wa kisiasa na 
kiuchumi. Wasikubali kuyumbishwa na mbinu ovu kama hizi ambazo zimelenga
 kutupotezea lengo la kuhoji masuala ya msingi kama ufaulu hafifu wa 
matokeo ya Kidato cha nne Mkoa wa Dar Es Salaam, hali ya chakula nchini 
(njaa),zilipo milioni 50 za kila kijiji zilizoahidiwa , upatikanaji wa 
Tume huru ya Uchaguzi,Katiba Mpya na hali mbaya ya kiuchumi kwa wananchi
 .
Mwisho Kamati Ndogo ya Kamati Kuu inawashukuru watanzania wote kwa 
kuendelea kuunga mkono jitihada za kupambana na udikteta nchini na 
inawaomba waendelee kuwakumbuka kwa sala/dua viongozi mbalimbali wa 
Chama waliopo kwenye mateso ya kesi, mahabusu na wengine wanatumikia 
vifungo kutokana na kuonewa na watawala.
……………………
Prof. Abdalah Jumbe Safari
Makamu Mwenyekiti Taifa –Bara
16 Februari, 2017
Prof. Abdalah Jumbe Safari
Makamu Mwenyekiti Taifa –Bara
16 Februari, 2017







0 comments:
Chapisha Maoni