Chama
 cha Madaktari Tanzania (MAT) kimesema Chuo Kikuu cha Kimataifa cha 
Matibabu na Teknolojia (IMTU)  sanjari na hospitali iliyo chini yake, 
vinastahili kufungiwa.
Tamko
 hilo la chama limekuja huku mamlaka mbalimbali zinazohusika na 
usimamizi wa karibu wa vyuo vikuu vya matibabu zikikiweka chuo hicho 
kiporo,  kusubiri uchunguzi wa tuhuma zinazokikabili za kutupa viungo 
vya binadamu jalalani, ukamilike kabla ya kuchukua hatua zinazostahili.
Kitendo
 hicho cha kutupa viungo vya binadamu jalalani kimetajwa na watu 
mbalimbali, wakiwemo wataalamu kuwa ni cha  ajabu kinachodhalilisha nchi
 na utu wa binadamu.
Akizungumza
 na mwandishi wa habari hizi, alisema taasisi hiyo isingetakiwa kutoa 
mafunzo ya udaktari wala kufanya tafiti zozote, ikiwa ni pamoja na 
kutoruhusiwa kutoa huduma za afya  katika hospitali yake.
Mwingine
 aliyezungumzia sakata hilo ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge 
ya Huduma za Jamii, Margareth Sitta aliyepongeza taasisi za serikali kwa
 hatua za haraka walizochukua kuhakikisha watu hao wanabainika mapema na
 kukamatwa.
Hata
 hivyo, Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii pamoja na Tume ya Vyuo Vikuu 
(TCU) kwa nyakati tofauti, walisisitiza nia yao ya kuchukua hatua dhidi 
ya chuo hicho, mara jopo linalochunguza sakata hilo litakapokamilisha 
kazi yake. 
Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Kebwe Stephen alisema kwamba amesikitishwa na kitendo hicho ambacho si cha kawaida.
Alitaka  upelelezi ufanyike haraka, adhabu stahiki ichukuliwe kutokana na kitendo hicho.
  “Baada
 ya kukamilika kwa upelelezi wa tukio hili na kupata taarifa za kwa nini
 walifikia hatua hii, naahidi wizara yangu itachukua hatua kali,” alisema Kebwe.
Katika
 mkutano na waandishi wa habari jijini Dar es  Salaam jana, msemaji  wa 
wizara hiyo, Nsachris Mwamwaja alisema kutokana na kuwa jambo hilo ni 
jipya, wataangalia uwezekano wa kuchukua hatua kwa mujibu wa sheria za 
nchi.
Alisema
 ingawa wizara yake haihusiki na usimamizi wa vyuo hivyo vinavyozalisha 
madakatri na kutaka waulizwe TCU, kwa mujibu wa Mwamwaja, kitendo 
walichofanya madaktari husika si cha kimaadili.
Alisema pamoja na kuwa kitendo hicho si cha maadili pia wanaangalia madhara ya kiafya kulingana na tukio hilo.
“Lakini
 pia ni vema kuangalia na jiji (Dar es Salaam) ni jinsi gani wanasimamia
 madampo yao, kwa nini inaruhusu kumwaga uchafu wowote bila kuwepo 
wakaguzi au ni utaratibu gani wanatumia kulinda afya za wananchi,”alisema  Mwamwaja.
Kwa
 upande wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi yenye dhamana na vyuo 
vikuu, Katibu Mkuu wake,  Profesa  Sifuni Mchome alisema pia wanasubiri 
ripoti  ya timu iliyoundwa kuchunguza suala hilo wachukue hatua za 
haraka chini ya Tume ya Vyuo Vikuu (TCU).
“Kwa sasa uchunguzi unaendelea hivyo hatuwezi kuchukua hatua yoyote,” alisema Profesa Mchome. Katibu Mkuu alisema katika tume hiyo iliyoundwa na polisi, yumo  mwakilishi wa elimu kutoka TCU.
Alisisitiza
 wataangalia suala hilo na kupendekeza hatua za kuchukua kutokana na kwa
 sasa hakuna sheria inayowabana kutokana na kuwa suala hilo ni jipya 
nchini.
Akizungumzia
 tukio hilo, Ofisa Habari Mwandamizi wa TCU, Edward Mkaku alisema 
wanasimamia ubora wa elimu ya juu na suala lililotokea ni kesi ya chuo 
kwa asilimia 100.
Hata
 hivyo, alisema kwa kuwa Mkurugenzi wa Ithibati wa Elimu ya Juu katika 
tume hiyo yupo kwenye tume iliyoundwa, wataangalia hatua za kuchukua 
baada ya uchunguzi kukamilika.
Alisema
 TCU ni taasisi yenye utaratibu, hivyo itatoa uamuzi baada ya ripoti kwa
 kuwa sasa IMTU bado ni watuhumiwa na haipaswi kuhukumiwa.
“Tunasubiri
 tume imalize uchunguzi ndipo tutaona tutachukua hatua gani kulingana 
na  Sheria ya Vyuo Vikuu kwani kwa sasa sheria ya suala hilo haipo 
kutokana na kwamba ni jipya kutokea nchini,”alisema.
Wakili
 wa Kujitegemea kutoka MK Law Chambers, Karoli Mluge akizungumza nafasi 
ya sheria katika suala hilo, alisema hakuna sheria inayozungumzia kwamba
 kutupa viungo vya binadamu au mwili hadharani ni kosa.
Mluge
 alisema  jamii lazima itofautishe Sheria na suala zima la maadili na 
ubinadamu. Alisema kibinadamu na maadili, utupaji wa viungo vya binadamu
 si sahihi na ni jambo linaloshitua lakini  kisheria, haimtii mtu 
hatiani .
“Kimaadili si sawa, lakini suala hili ni la kiubinadamu  halina sheria,” alisisitiza.
 Alisema hata mtu anapokutwa na kiungo cha binadamu, hatiwi hatiani kwa 
maana ya kukutwa na kiungo husika isipokuwa, kinachotafutwa ni 
kujiridhisha ni kwamba amekipataje kutoka mwili wa binadamu.
“Si kosa kukutwa na kiungo cha binadamu…cha msingi, ni kuthibitisha umekipataje,” alisema. 
Kumekuwepo
 maswali juu ya ni namna gani vyuo vinapata miili ya kufanyia mafunzo 
kwa vitendo na baada ya mafunzo inapaswa iteketezwe namna gani. Hata 
hivyo katika kutafuta ufafanuzi wa maswali haya, taasisi hizo 
zinazohusika na usimamizi wa vyuo hazikuwa tayari kuzungumzia kwa undani
 suala hilo, kwa madai ya kusubiri matokeo ya tume iliyoundwa.
Tume
 hiyo iliyoundwa, kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar 
es Salaam, itahakikisha inakuja na majibu, ikiwa ni pamoja na kujua 
idadi kamili ya watu wenye viungo hivyo.
Timu
 hiyo ya wataalamu ya watu saba inayohusisha pia Mkemia Mkuu wa 
serikali, itakuja na majibu viungo hivyo ni vya muda gani na zilitumika 
kemikali gani kuvikausha.
Jopo
 litabaini pia  kama ipo sheria na ni ipi  inavunjwa. Inalenga kubaini 
pia kama upo uzembe katika kulinda viungo vya binadamu na vinapatikanaje
 kwa ajili ya mazoezi.
Katika
 sakata hilo lililovuta hisia za watu na kuzua mjadala mitaani na kwenye
 mitandao ya kijamii, watu wanane wakiwemo Madaktari wa IMTU, 
walikamatwa juzi na Polisi kwa mahojiano wakituhumiwa kuhusika  katika  
utupaji viungo vya binadamu jalalani.
Polisi
 ilisema mifuko ipatayo 85 yenye vichwa, miguu, mikono, moyo, mapafu, 
vifua na mifupa ya aina mbalimbali ya binadamu, ilikutwa maeneo ya bonde
 la Mbweni Mpiji, eneo la Bunju jijini Dar es Salaam.






 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
0 comments:
Chapisha Maoni