Mgombea urais wa Zanzibar kupitia Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif 
Sharif Hamad, amesema CUF inaendelea kutafuta haki ya Wazanzibar ya 
kutaka Tume ya Uchaguzi Zanzibar (Zec) kuendelea kutangaza matokeo ya 
uchaguzi ili mshindi ajulikane na hatimaye kuapishwa.
Aliyasema hayo wakati akizungumza na wafuasi wa chama hicho katika makao
 makuu ya CUF Mtendeni juzi, baada ya kurudi safari yake ya kuonana na 
rais wa awamu ya nne, Dk. Jakaya Kikwete, Ikulu, jijini Dar es Salaam.
Aliwaambia wanachama hao kuwa hakuna kurudi nyuma katika kudai haki yao 
kwa njia ya amani na utulivu ili matokeo yatangazwe na mshindi wa urais 
ajulikane.
“Niwahakikishieni vijana na wanachama wa CUF kuwa hakuna kurudi nyuma, 
tunaendelea kudai haki yetu na tunashukuru dunia nzima inatuunga mkono 
kwa hili,”alisema Maalim Seif, ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais wa
 Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar (SUK).
Alisema kuwa wapinzani wao, Chama Cha Mapinduzi (CCM) mpango wao ni 
kutaka kuendelea kuwa katika madaraka wakijua kuwa muda wa Dk. Ali 
Mohammed Shein wa kukaa madarakani umekwisha, lakini wanang’ang’ania 
aendelee kinyume cha Katiba.
Aidha, alisema kuwa hakuna dawa yoyote ya kumaliza mgogoro ulipo 
Zanzibar isipokuwa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (Zec) kuendelea kutoa 
matokeo ya uchaguzi wa Oktoba 25, mwaka huu ili mshindi ajulikane na 
kuapishwa.
“Wanaosema kuwa uchaguzi urejewe waachieni wenyewe, sisi katika CUF 
hakuna msamiati huo kwa sasa kurejea uchaguzi, huo ndio msimamo wetu,” 
alisisitiza Maalim Seif.
Alisema kuwa kwa uwezo wa Mungu haki yao wataipata na kuwataka vijana 
kuendelea kuwa watulivu na kuendelea kutunza amani ya nchi kwa 
kutokubali kuchokozeka. Alisema CUF na viongozi wake hawatakubali kuwa 
chanzo cha kuvuruga amani ya nchi na wataendelea kuhubiri amani wakati 
wote.
Mvutano wa kisiasa unaoendelea Zanzibar ulisababishwa na Mwenyekiti wa 
Zec, Jecha Salim Jecha, kutangaza kufuta uchaguzi wa Zanzibar wa rais na
 wawakilishi Oktoba 28, kwa madai kuwa ilibaini kuwapo kwa kasoro kadhaa
 kisiwani Pemba.
Hata hivyo, waangalizi wa nje na ndani wameeleza kushangazwa ha hatua ya
 Jecha, kwa kuwa hawakushuhudia kasoro zozote hadi walipotoa ripoti ya 
awali.
Aidha, asasi za nchini na mataifa kadhaa yakiwamo Uingereza, Ireland na 
Marekani yameshatoa taarifa ya kushangazwa na uamuzi wa Jecha na 
kushauri mchakato wa kutangaza matokeo uendelee.
MTOTO WA KARUME AIBUA MAPYA
Mjadala kuhusiana na hatma ya Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar uliofutwa na 
Jecha, umechukua sura mpya, baada ya mmoja wa watoto wa Rais wa zamani, 
Dk. Amani Abeid Karume, kuibuka na kufichua kile anachoamini kuwa ni 
sababu ya utata uliojitokeza sasa.
Mtoto huyo ni Mwanasheria, Fatma Karume, ambaye akiwa pamoja na Rais wa 
Chama cha Wanasheria wa Zanzibar (ZLS), Awadh Ali Said, waliuambia umma 
kupitia mahojiano ya moja kwa moja kwenye kituo kimoja cha televisheni 
jijini Dar es Salaam juzi kuwa sababu mojawapo ya kufutwa kwa uchaguzi 
wa Zanzibar ni muundo wa uongozi unaomruhusu rais wa visiwa hivyo kuwa 
mmoja wa wajumbe katika Baraza la Mawaziri la Serikali ya Jamhuri ya 
Muungano wa Tanzania.
Akifafanua, Fatma alisema kuwapo kwa nafasi ya moja kwa moja ya Rais wa 
Zanzibar kwenye Baraza la Mawaziri kunaibua mgongano inapotokea mshindi 
wa upande mmoja akiwa ni wa kutoka chama kingine na hiyo ni sababu 
mojawapo wanayoamini kuwa imechangia kufutwa kwa uchaguzi na pia kukwaza
 ukuaji wa demokrasia visiwani humo.
Alisema ni dhahiri hali huwa ngumu kwa baraza la mawaziri linaloundwa na
 watu wa itikadi ya chama kimoja kuchanganyika na mwingine mwenye 
itikadi tofauti, hasa katika mazingira ya kuwa na usiri katika baadhi ya
 mambo na kwamba, hilo huchangia kusuasua kwa maendeleo ya kidemokrasia 
visiwani Zanzibar.
Hata hivyo, ili kuondokana na mgogoro kama uliopo sasa, Fatma alisema ni
 muhimu kwa viongozi wa kisiasa nchini na kwingineko barani Afrika 
kuzingatia sheria na katiba zilizopo.
Awali, ilisisitizwa na wanasheria hao kuwa uamuzi wa kufutwa kwa 
uchaguzi wa Zanzibar uliochukuliwa na Mwenyekiti wa Zec peke yake, 
haukuzingatia sheria na katiba na ndiyo maana sasa kumeibuka mgogoro wa 
kikatiba kwani kifungu kinachotumika kuhalalisha hoja ya kuendelea 
kubaki madarakani kwa Dk. Shein kimekuwa kikitafsiriwa vibaya kwa 
maslahi ya kisiasa.
Akielezea zaidi, Awadh alisema hakuna kifungu chochote kinachomruhusu 
Jecha kufuta uchaguzi na ndiyo maana hadi sasa hakuna mtu aliyethubutu 
kutaja kwa uwazi ni sheria ipi imempa nguvu mwenyekiti huyo wa Zec 
kufuta uchaguzi wa Zanzibar.
Source: Nipashe
Ijumaa, 6 Novemba 2015
Home »
 » Maalim Seif Aweka Ngumu Adai Hawawezi Kurudia Uchaguzi Zanzibar







 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
0 comments:
Chapisha Maoni