Jaji Mkuu mstaafu Othman Chande ameteuliwa kuongoza jopo la wataalamu 
watakaochunguza mazingira yaliyosababisha ajali ya ndege iliyomuua 
aliyekuwa katibu mkuu wa umoja huo, Dag Hammarskjold.
Uteuzi huo wa jaji mkuu mstaafu umefanywa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN), Antonio Guterres.
Hammarskjold alipoteza maisha katika ajali ya ndege iliyotokea Zambia 
mwaka 1961 wakati akitokea Congo ambayo ndiyo kwanza ilikuwa imepata 
uhuru.
Hammarskjold alikuwa nchini humo kwa ajili ya ujumbe wa amani.
Naibu msemaji wa UN, Farhan Haq amesema Chande ataongoza jopo hilo 
ambalo litakuwa na kazi kupitia taarifa zilizoandaliwa na wachunguzi 
waliopewa jukumu na katibu mkuu mstaafu, Ban Ki-moon.
Uchunguzi huo unafuatia azimio la Umoja wa Mataifa lililopitishwa na 
Baraza Kuu ambalo lilipendekezwa kufanyika uchunguzi wa kina kubaini 
mazingira ya ajali hiyo.
Awali, kulikuwa na ripoti kuwa Uingereza na Marekani zilikuwa zimegoma 
kutoa baadhi ya taarifa muhimu kuhusu tukio hilo, huku Afrika Kusini 
ikilalamikiwa kwa kushindwa kutoa majibu kwa baadhi ya hoja.
Ripoti iliyotolewa na wataalamu huru waliochunguza ajali hiyo inaeleza 
kuwa Hammarskjold aliuawa baada ya kunusurika kwenye ajali hiyo. 
Kumekuwa na taarifa kuwa ndege hiyo ilishambuliwa.
Jopo hilo linaloongozwa na Chande linatarajia  kuanza kazi mara moja na 
kwamba litakuwa na jukumu la kupitia nyaraka zote, ikiwamo ripoti ya 
kurasa 99 iliyoandaliwa na wataalamu wa awali waliochunguza mazingira ya
 ajali hiyo.







 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
0 comments:
Chapisha Maoni