Paul Makonda Afunguka Kuitwa na Bunge Kwa Ajili ya Kuhojiwa
MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amesema hawezi kufika mbele 
ya Kamati ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge kuhojiwa kwa kuwa 
hajapokea barua ya kuitwa.
Akizungumza  jana jijini Dar es Salaam, Makonda alisema hatoweza kwenda 
mbele ya kamati hiyo bila barua rasmi iliyomtaka kufanya hivyo.
Bunge lililokuwa likiendelea na vikao vyake Dodoma kabla ya kuahirishwa 
juzi, lilipitisha uamuzi wa kuwataka Makonda na Mkuu wa Wilaya ya 
Arumeru, Alaxander Mnyeti, kufika mbele ya kamati hiyo na kuhojiwa 
kutokana na kauli walizozitoa, zinazodaiwa kuudharau mhimili huo wa 
dola.
Lakini Makonda alisema jana “hilo suala la mimi kuitwa kwenye kamati nalisikia na kulisoma kwenye magazeti."
"Sina uhakika ni lini wamefikia uamuzi huu wa kuniita na hata kama wamefikia uamuzi huo, sijaletewa barua rasmi.”
Baada ya Bunge kupitisha uamuzi huo wa kuitaka Ofisi ya Bunge iwaandikie
 barua viongozi hao, juzi baadhi ya wabunge walihoji kauli ya Katibu wa 
Bunge, Dk. Thomas Kashililah, kwamba azimio la chombo hicho cha kutunga 
sheria kumtaka Makonda kufika mbele ya kamati kujieleza kuhusu tuhuma za
 kuudharau mhimili huo, halikufuata utaratibu.
Hatua hiyo iliamsha hasira kwa baadhi ya Wabunge na kuomba mwongozo 
kuhoji kwa nini Katibu wa Bunge ametoa kauli ambayo inakinzana na 
makubaliano ya Bunge.
Mbunge wa Ukonga, Mwita Waitara na mwezake wa Iringa Mjini Mchungaji 
Peter Msigwa (wote Chadema) walihoji kuhusu kauli ya Dk. Kashililah.
Waitara alisema, “Asubuhi ya leo ( juzi) nimetumiwa ‘clip’ ya sauti ya 
Katibu wa Bunge akikosoa uamuzi wetu hapa na pia gazeti la Habari Leo, 
Ukurasa wa 25, kuna habari imeandikwa.
Katika taarifa hii, Katibu wa Bunge anasema maazimio ya Bunge yalikosewa
 na hayakufuata utaratibu,” alisema na kuongeza kuwa: “ Kwa maana 
nyingine, hatatekeleza kile tulichokubaliana.”
Mchungaji Msigwa wakati akichangia taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge 
ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama, alieleza kuwa hajafurahishwa na 
kauli ya Katibu wa Bunge.
Alisema Katibu wa Bunge amekosea kwenda katika vyombo vya habari na 
kudai chombo hicho cha kutunga sheria kimekosea kwa kuwa anafanya kazi 
ya Bunge na kwamba hajaajiri wabunge na anapaswa kufuata maagizo yao.
Hoja ya kutaka kina Makonda washughulikiwe iliwasilishwa na Mbunge wa 
Ukonga, Mwita Waitara (Chadema) katikati ya wiki na ilijadiliwa na 
kuungwa mkono na wabunge wote, wakiwamo mawaziri kwa kusema ‘ndiyo’.







 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
0 comments:
Chapisha Maoni